Story
Mtakatifu Abanoub Mtoto Shahidi Abanoub alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili tu alipouawa kama shahidi na mtawala Mrumi. Tarehe 31 Julai, Kanisa letu huadhimisha kifo chake, kama siku ya kuzaliwa kwake katika uzima wa milele.
Masalio ya Mtakatifu Abanoub, pamoja na masalio ya Wakristo wengi waliouawa pamoja naye, bado yamehifadhiwa hata leo katika kanisa la Bikira Maria Mtakatifu na Mtakatifu Abanoub katika mji wa Samanoud. Inasemekana pia kwamba Familia Takatifu ilitembelea mahali hapo wakati wa Kukimbilia kwao Misri. Kanisa hilo bado lina kisima ambacho Bwana Yesu, Mtakatifu Maria, na Mtakatifu Yosefu walikinywea maji. Maonekano na miujiza mingi bado hutokea katika kanisa hilo hata siku hii ya leo. Abanoub alizaliwa katika mji uitwao Nehisa katika Delta ya Mto Nile. Alikuwa mwana pekee wa wazazi wema Wakristo waliofariki alipokuwa bado mtoto mdogo. Akiwa na umri wa miaka kumi na miwili, Abanoub aliingia kanisani na kumsikia kasisi akiwaomba waumini wabaki imara katika imani wakati wa mateso yaliyochochewa na Diocletiano, mfalme Mrumi.
Abanoub alipokea Sakramenti Takatifu, kisha akamwomba Mungu amwongoze mahali ambapo angeweza kuikiri imani yake kwa Yesu Bwana wetu. Baada ya hayo Abanoub akatoka nje, na akawapa wahitaji vitu vyake vyote. Kisha akaanza safari kwa miguu kuelekea mji uitwao Samanoud. Alipokuwa akitembea, akamwona Malaika Mkuu Mikaeli katika utukufu wa mbinguni. Maono hayo yalikuwa ya ajabu sana hata Abanoub akaanguka chini, lakini Malaika Mkuu akamwinua, na akamwambia kwamba ni lazima ateseke kwa siku tatu huko Samanoud na kwamba angemshuhudia Yesu Kristo katika mahali pengine pia.
Alipofika Samanoud, Abanoub akamwendea mtawala Mrumi na kuitangaza imani yake wazi wazi. Pia akavitukana vinyago vya mtawala. Mtawala akakasirika na akatoa amri achapwe mjeledi tumboni mwake. Askari wakampiga Abanoub vibaya sana hata matumbo yake yakatoka nje ya tumbo lake. Lakini Malaika Mkuu Mikaeli akamponya kwa muujiza. Kisha mtawala akamtia gerezani pamoja na Wakristo wengine waliotiwa moyo na uwepo wake kati yao, na baadaye wakauawa kama mashahidi kwa ajili ya jina la Yesu.
Siku iliyofuata, mtawala akamchukua Abanoub katika mashua kuelekea mji uitwao Atrib, na kama adhabu, akamtundika Abanoub kichwa chini kutoka kwenye tanga la mashua. Askari, pamoja na mtawala wao, wakaanza kunywa na kucheza ngoma na kumpiga Abanoub mdomoni. Pua ya Abanoub ikatoka damu, lakini ghafla, askari wakapofuka na mtawala akapooza. Katika maumivu yao wakamlilia wakisema, "Tafadhali Abanoub, mwombe Mungu wako atuponye. Maana tukiponywa, tutakuwa Wakristo."
Mtakatifu Abanoub akajibu, "Hili litatokea tu huko Atrib, ili kila mtu huko ajue kwamba hakuna Mungu mwingine ila Kristo." Walipofika Atrib, wote wakaponywa, nao wakalia kwa furaha, "Sisi ni Wakristo! Tunamwamini Mungu wa Abanoub." Kisha wakavua sare zao na kuzitupa chini mbele ya mtawala wa Atrib. Liwali akakasirika sana, na akatoa amri wauawe.
Huko Atrib, Abanoub aliteswa vibaya sana, mara kwa kuchapwa mjeledi na mara kwa kufungwa kwenye kitanda cha chuma na kuwashiwa moto chini yake. Lakini katika dhiki hizi zote, Bwana akadhihirisha nguvu zake na Abanoub akaokolewa. Kutokana na miujiza hii, watazamaji wengi wakawa Wakristo, na wakapokea taji ya ushahidi. Kisha mtawala akatoa amri zikatwe mikono na miguu ya Abanoub. Ghafla Malaika wa Bwana akashuka kutoka mbinguni, akaiweka mikono na miguu mahali pake, na akamponya. Kisha Abanoub akainuka na kutembea mbele ya kila mtu. Mamia ya watu wakawa Wakristo kutokana na muujiza huo.
Akiwa amechanganyikiwa, mtawala akawaita baadhi ya wachawi bora zaidi nchini, na akawaomba wamsaidie kumshinda Abanoub. Wakapendekeza kwamba atupwe kwa nyoka wenye sumu. "Nyoka hao wana sumu ya kutosha kuua watu mia mbili au mia tatu," wakasema. Hivyo wakamtia Abanoub katika chumba pamoja na nyoka, lakini Mungu, aliyeyafunga vinywa vya simba katika wakati wa Danieli, akawafuga nyoka nao hawakumdhuru Abanoub. Asubuhi, na kwa mshangao wa kila mtu, Mtakatifu Abanoub akatoka chumbani akiwa hai. Kisha ghafla mmoja wa nyoka akatambaa kutoka chumbani na kujizungusha kwenye shingo ya mtawala.
Mtu yule akaanza kutetemeka naye akalia, "Kwa jina la Yesu Mungu wako, unirehemu na usiache nyoka anidhuru." Mtakatifu aliyependa kila mtu — rafiki au adui — kama vile Injili inavyoamuru, akaomba kutoka moyoni, kisha akamwamuru nyoka ashuke na asimdhuru mtawala. Siku hiyo, watu wengi waliokuwepo, pamoja na wachawi watatu, wakamwamini Yesu.
Hatimaye mmoja wa washauri wa mtawala akamwambia amkate kichwa mtakatifu na kumaliza kisa hiki. Hivyo mtawala akawaamuru askari wamuue Mtakatifu Abanoub kwa upanga. Mtu mwaminifu aitwaye Mtakatifu Julio akaufunga mwili wa Abanoub kwa kitani safi na akampeleka kwenye mji wake wa nyumbani Nehisa ambako alizikwa.
Mwaka 960 B.K., mwili wake ulihamishiwa kwenye kanisa la Bikira Maria Mtakatifu huko Samanoud ambako bado unalala hata leo. Katika kipindi cha miaka, Abanoub alifanya maonekano mengi katika kanisa hilo. Alikuwa akijidhihirisha kama mtoto wa miaka kumi na miwili na kucheza na watoto wenye umri wake. Mara moja aliingilia mgomvi kati ya baadhi ya watoto Wakristo na Waislamu. Tukio hili likamkasirisha mmoja wa Waislamu mashuhuri waliokuwa wakiishi kando ya kanisa. Kasisi wa kanisa, aliyekuwa mzee, alikasirika alipojua yaliyotokea. Katika hasira yake akamzuia Mtoto Mtakatifu asionekane. Kwa ajabu, Mtakatifu aliitii amri ya kasisi na maonekano yakakoma kwa miaka mingi.
Ilikuwa tu mwaka 1974, wakati Padri Abanoub Louis alipowekwa wakfu kuwa kasisi katika kanisa hilo, ndipo akawaita maaskofu wawili waliokuja kanisani na baada ya kuomba kwa bidii, wakampa ruhusa mtakatifu aonekane endapo angetaka. Baada ya wiki mbili hivi, onekano la kwanza likashuhudiwa, likafuatiwa na miujiza na maonekano mengi.
Askofu mmoja mashuhuri alitembelea Montreal hivi karibuni na akazungumza kuhusu miujiza aliyoishuhudia mwenyewe. Alisema, "Siku moja, nilikuwa nikitembelea Samanoud, nami nikashiriki katika kuadhimisha misa katika kanisa la Bikira Maria Mtakatifu na Mtakatifu Abanoub. Misa ilikuwa katikati ya wiki, na ilihudhuriwa na watu wachache. Tulipomaliza, nilieleza jinsi lilivyo kanisa zuri, na kwamba nilifurahia sana kuomba misa ndani yake, isipokuwa jambo dogo moja." Niliongeza kwamba katika muda wote wa sala, mvulana mdogo aliendelea kuingia na kutoka kupitia mlango wa mbele. Kasisi aliniambia kwamba hakuona watoto wadogo wowote, na kwamba misa ilihudhuriwa na watu wazima wachache. Kisha akahitimisha kwamba mvulana yule mdogo alikuwa Mtakatifu Abanoub.
Mtu mwingine alisema kwamba baada ya kuhudhuria misa, alianza safari yake akiwa amebeba mkoba. "Ilikuwa ikinyesha mvua, nikateleza, nikaanguka ndani ya kidimbwi cha maji. Kisha mvulana mdogo akaja akinikimbilia, na akanisaidia kusimama. Akanikabidhi mkoba wangu, na akaniambia nivuke hadi upande mwingine wa barabara. Nilishangaa kugundua kwamba nguo zangu na mkoba wangu vilikuwa vimekauka kabisa. Kisha nikamtafuta yule mvulana mdogo, lakini alikuwa ametoweka."
Sala na maombi ya Shahidi huyu mkuu, Mtoto Mtakatifu Abanoub, na yawe pamoja nasi. Amina.